Kushirikiana na upagani ni kosa lililo waghalimu Waisraeli
TUJIFUNZE KUTOKANA NA MAKOSA YA WAISRAELI
Na Ndikumana Issaya
WAISRAELI walipokuwa wakiingia katika Nchi ya Ahadi, walijua mambo ambayo Yehova alitaka wafanye. Mungu alikuwa amewaamuru hivi kupitia Musa: Mnapaswa kuwafukuzia mbali wakaaji wote wa nchi hiyo kutoka mbele yenu na kuharibu maumbo yao yote ya mawe, nanyi mnapaswa kuziharibu sanamu zao zote za madini ya kuyeyusha, na mnapaswa kupaharibu mahali pao pote palipoinuka.—Hes. 33:52.
Waisraeli hawakupaswa kufanya agano lolote na wakaaji wa nchi hiyo, wala hawakupaswa kufanya mapatano yoyote ya ndoa pamoja nao. (Kum. 7:2, 3) Kwa kweli, watu hao waliochaguliwa na Mungu walionywa hivi: “Jiangalie usije ukafanya agano pamoja na wakaaji wa nchi hiyo unayoiendea, isije ikawa mtego katikati yako.” (Kut. 34:12) Hata hivyo, Waisraeli hawakumtii Mungu na hivyo wakanaswa na mtego huo. Kwa nini walinaswa na mtego? Ni mambo gani yenye kuonya tunayoweza kujifunza kutokana na kisa chao?—1 Kor. 10:11.
Kushirikiana na Watu wa Mataifa Kuliwaongoza Kwenye Ibada ya Sanamu na kumkosea Mungu
Waisraeli waliwashinda wakaaji wa Nchi ya Ahadi na kuimiliki. Hata hivyo, wana wa Israeli hawakutii amri za Mungu kikamilifu. Hawakuwafukuzia mbali maadui. (Amu. 1:1–2:10) Badala yake, Waisraeli walipoanza kukaa katikati ya “mataifa saba” ambayo yalikuwa katika nchi hiyo, walishirikiana kwa kawaida ya watu wa mataifa hayo na hivyo wakaanzisha urafiki nao. (Kum. 7:1) Matokeo yalikuwa nini kwa Waisraeli? Biblia inasema: “Wakaanza kuoa binti zao, na binti zao wenyewe wakawapa wana wao, nao wakaanza kuitumikia miungu yao. Basi wana wa Israeli wakafanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova, wakamsahau Yehova Mungu wao, wakatumikia Mabaali.” (Amu. 3:5-7) Baada ya kushirikiana na watu wa nchi hiyo, Waisraeli walianza kuoana nao na kuabudu sanamu zao. Baada ya Waisraeli kufanya mapatano ya ndoa nao, ikawa vigumu sana kwa Waisraeli kuwafukuza wapagani hao kutoka katika nchi hiyo. Ibada ya kweli ilichafuliwa, na Waisraeli wenyewe walianza kuitumikia miungu pamoja na kupokea desturi na mafundisho potofu yaliyo toka katika upagani wa hayo mataifa.
Wakiwa marafiki wao, wakaaji wa Nchi ya Ahadi walihatarisha hata zaidi hali ya kiroho ya Waisraeli kuliko walipokuwa maadui wao. Fikiria jambo lingine ambalo huenda lilichafua ibada yao.
Walipoingia katika Nchi ya Ahadi, wana wa Israeli waliacha maisha ya kuhamahama na wengi wakawa wakulima. Huenda walitumia njia za ukulima kama za watu walioilima nchi hiyo kabla yao. Inaonekana kwamba hawakufuata tu njia za ukulima za Wakanaani. Waliposhirikiana na wakaaji hao, Waisraeli walishawishiwa pia kukubali ibada yao na matambiko ya kipagani katika kilimo.
Wakanaani waliabudu Mabaali wengi—miungu ambayo ilisemekana kwamba iliufanya udongo uwe na rutuba. Zaidi ya kulima na kuvuna mazao, baada ya muda Waisraeli walijiunga nao katika kuheshimu miungu ya Wakanaani ambayo walidai ilileta mazao mengi. Kwa hiyo, watu wengi wa Israeli walijifanya wanamwabudu Yehova, lakini kwa kweli walishiriki kabisa katika uasi wa imani.
Onyo Kali Kwetu Leo
Haielekei kwamba Waisraeli walikusudia kushiriki katika ibada ya Baali na matendo yake mapotovu walipokutana kwa mara ya kwanza na wakaaji wa Nchi ya Ahadi. Hata hivyo, kushirikiana na watu hao kuliwaongoza katika mambo hayo. Tukishirikiana na watu ambao huenda ni wenye urafiki lakini hawafuati imani, maadili, na kanuni zetu za Kikristo, je, hatutapata madhara kama hayo? Bila shaka, huenda tukalazimika kushirikiana na watu wasio waamini katika mambo fulani kazini, shuleni, au labda hata nyumbani na isiwe na athari kiroho, lakini ni hatari kubwa kushirikiana na watu wasio amini katika mambo ya imani. Hata hivyo, mambo yaliyowapata Waisraeli ni onyo kwetu kwamba tukitafuta umoja na ushirikiano wa aina hiyo tunacheza na moto. Biblia inasema ukweli huu usioepukika: “Mazungumzo mabaya huharibu tabia njema.”—1 Kor. 15:33.
Leo, tunakabili matatizo mengi kanisani kama ya Waisraeli. Katika jamii ya leo, kuna vitu vingi na watu ambao wanaabudiwa kama sanamu. Wanaabudu pesa, watu mashuhuri katika burudani, wanamichezo, mifumo ya kisiasa, viongozi fulani wa kidini, na hata washiriki wa familia. Chochote ambacho mtu anaabudu kinaweza kuwa jambo kuu katika maisha yetu. Kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na wale ambao hawampendi Yesu Kristo katika kufuata maagizo yake kunaweza kutudhuru kiroho.
Desturi potofu na haramu ilikuwa sehemu kuu ya ibada ya Baali na iliwavutia na kuwashawishi Waisraeli wengi. Watu wengi wa Mungu leo bado wananaswa na mitego kama hiyo.
Uamuzi wa kutii yale ambayo Mungu anasema kuhusu kutoshirikiana na watu wasio amini, ilipaswa kuvuta usikivu wetu kwa kiasi kikubwa na kuwekwa kuwa kipaumbele chetu katika safari yetu ya kiroho. (Kum. 30:19, 20)
Hivyo, tunahitaji kujiuliza hivi: ‘Ninashirikiana na nani katika tafrija na sherehe? Wanafuata viwango gani vya maadili? Je, wanamwabudu Mungu wa kweli? Je, nitakuwa Mkristo bora nikishirikiana nao?’ Je, mafundisho yao yamejengwa katika neno la Mungu?
Mtunga-zaburi aliimba hivi: Wenye furaha ni wale wasio na kosa katika njia yao, wale wanaotembea katika sheria ya Mungu. Wenye furaha ni wale wanaoshika maagizo yake; wanaendelea kumtafuta kwa moyo wote.” (Zab. 119:1, 2) Kwa kweli, “mwenye furaha ni kila mtu anayemwogopa Mungu na hukumu zake. Anayetembea katika njia zake.” (Zab. 128:1)
Ni muhuimu sana kuchunguza kwa umakini hasa linapokuja suala la kuanzisha umoja na ushirikiano katika mambo ya kiroho. Uamuzi wetu utafaa ikiwa utajikita katika maandiko matakatifu huko tukijitenga na kila imani potofu. Mithali. 13:20. Pia ni muhimu tujifunze kutokana na makosa ya Waisraeli na hivyo tumtii Mungu kabisa.
Mungu akubariki sana wewe uliye tumia muda wako katika kufuatilia somo hili. Tuandikie maoni yako hapo chini.

COMMENTS